KWANINI UPYAISHO WA KARISMATIKI KATOLIKI UNAUSISHWA NA MADHEHEBU MENGINE
Kwa nini Upyaisho wa Karismatiki Katoliki unahusishwa na madhehebu ya Kiprotestanti na upentekoste wa kilokole.?
Tunasoma katika Yoh 3:8 kwamba “Upepo huvuma upendako na sauti yake waijua lakini hujui unakotoka wala unakokwenda...”
Baada ya John Wesley mwanzilishi wa makanisa ya kimethodist kufariki na ambaye pia anaonekana kuhimiza juu ya utakatifu wa maisha na kuhubiri injili kwa nguvu za Roho Mtakatifu miaka ya 1700s ubaridi na ukimya uliendelea hadi Sr Elena Guera alipopata msukumo wa kuhimiza tena juu ya Roho Mtakatifu ndani ya Kanisa Katoliki mwaka 1895.
Baada ya barua za Sista huyu kujibiwa na Baba mtakatifu Leo XIII ndipo ilipotungwa sala ya “uje Roho Mtakatifu” na kuanza kusaliwa na waamini.
Ukimya uliendelea kutawala ndani ya Kanisa na hapakuwa na mkazo tena Juu ya Roho Mtakatifu na namna ya kuishi maisha binafsi na kuhusiana na Mungu kwa namna ya kipekee.
Wakati huo ikumbukwe kuwa mwaka 1901 ndipo vuguvugu la upentekoste lilianza rasmi na kuenea sehemu mbali mbali ulimwenguni likiongozwa na mwinjilisti Charles Parham.
Ni wazi kuwa ndani ya kanisa himizo la Roho Mtakatifu lilipoa baada ya Sr Elena na badala yake Upentekoste ukaanza kukolea katika madhehebu mengine.
Kimsingi hii ndio sababu kubwa wengi huiona Karismatiki kuwa na mizizi ya kipentekoste kwani jambo ambalo lilianza kuonekana kwetu halikupewa mkazo sana badala yake wengine walifunuliwa kwa namna yao na kulifanyia kazi na baadaye likarudi tena ndani ya Kanisa katoliki.
Maandalizi ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano
Katika kuandaa mtaguso huu ndipo tena baada ya miaka mingi kupita Baba Mtakatifu Yohane XXIII mwaka 1962 alisali tena akimwomba Mungu kupyaisha maisha ya wanakanisa kama katika Pentekoste ya kwanza.
Wikiendi ya Duquesne
Baada ya kumalizika kwa mtaguso wa pili wa vatikano 1965 ambapo pia kulikua na himizo juu ya kuhusiana binafsi na Mungu kwa namna ya kipekee na Roho Mtakatifu.
mwaka 1967- Tukio linalohesabiwa na wengi kuwa ni mwanzo wa Upyaisho Karismatiki Katoliki, ni tukio
linaloitwa kwa kiingereza ‘Duquesne Weekend’ (Mwisho wa Juma wa Dukeni). Hakika yako
matukio mengine ya mlipuko huu yaliyotokea wakati huo huo lakini tukio la Dukeni ndilo
lililoandikwa zaidi kuliko mengine.
Tukio la mwisho wa juma la Dukeni lilitokea hivi,
Kikundi cha wakufunzi walei wa Chuo Kikuu cha Dukeni kinachoendeshwa na Mapadre wa
Shirika la Roho Mtakatifu (Duquesne University of the Holy Spirit), huko Pittsburgh, Marekani,
walianza kukutana kwa miezi kadhaa wakijaribu kutafakari kile kinachopungua katika maisha yao
binafsi. Hatimaye hawa hatimaye hawa walivutiwa kuhudhuria mkutano wa sala wa Upyaisho
Karismatiki(waprotestant) uliokuwa ukiendeshwa na Waepiskopali katika eneo lao kama namna ya kujifunza.
Wawili kati yao walirudi kwenye mkutano huo juma moja baadaye na wakabatizwa katika Roho
Mtakatifu. Hawa wawili walikuwa mwanzo wa Ubatizo wa Roho mtakatifu kuwafikia
watu kadhaa hapo chuoni. Hatimaye wale waliopokea ubatizo wa Roho Mt. waliwaalika wengine wachache,
wengi wao wakiwa vijana wanafunzi katika mafungo ya mwisho wa juma (Februari 17-18,1967)
kwa lengo la kuwaombea Ubatizo katika Roho Mtakatifu. Hili ndilo tukio maarufu la mwisho wa
juma wa Dukeni.
Wale vijana wote wakabatizwa katika Roho Mtakatifu. Mmoja wao ni Patricia Galagher
Mansfield ambaye ambaye ameueleza ushuhuda wake mahali pengi. Mwezi mmoja
baadaye Machi, 1967, Ralph Martin, Steve Clark, Gerry Rauch na Jim Carvanar ambao walikuwa
viongozi wa kitaifa wa Kursilo(vugu vugu la kiroho), walitembelea Dukeni. Huko walikuta moto
umeanza na wao pia wakabatizwa katika Roho Mtakatifu. Baadaye hawa wane walirejea vituoni
kwao kwenye vyuo vikuu vya Michigan na Notre Dame ambako walisambaza mota na hivyo
Upyaisho Karismatiki Katoliki(UKK) ukaanza kuenea. UKK ulienea kwa kasi sana Marekani kote na
nje ya Marekani. Miaka minane baadaye Ralph Martin mmoja wa viongozi wa mwanzo kabisa
wa Upyaisho Karismatiki Katoliki aliarifu kwamba Upyaisho Karismatiki Katoliki sasa umeenea
karibu katika kila nchi duniani.
Kupokelewa na Vatikano
Mwezi Octoba 1973, Papa Paulo VI alifanya mkutano wa pekee na viongozi 13 walioshiriki
mkutano wa kimataifa wa viongozi wa Upyaisho Karismatiki Katoliki mjini Roma. Katika mkutano
huu Papa alisema maneno ya kutia moyo UKK. Katika mikutano na viongozi wa UKK , mapapa
Paulo VI na Yohani Paulo II, wameendelea kutia moyo na kufurahia utendaji wa UKK. Mwanzoni
mwa miaka ya sabini Papa Paulo VI alimuomba Leo Kardinali Suenens achukue jukumu la
kichungaji kwa UKK.
Mwaka 1993, hati maalumu ya kanisa ilitolewa nakatika kutambuliwa huko jina rasmi
likabadilishwa na kuwa ‘Huduma ya Kimataifa ya Upyaisho Karismatiki Katoliki’ (International
Catholic Charismatic Renewal Services – ICCRS).
Upyaisho Karismatiki Katoliki kote duniani hadi Tanzania
Hadi sasa UKKK umepokewa karibu katika nchi zote za dunia. Hapa Tanzania vikundi vya sala
vimeenea katika parokia nyingi kwa idhini ya maparoko na katika majimbo mengi maaskofu
wameonyesha ushirikiano , ukaribisho mkubwa na nia nzuri ya kutaka kusaidia kulea vuguvugu
hili.
Ni vyema ifahamike kuwa ukimya uliotawala katika kufanyia kazi kwa haraka upyaisho wa Roho Mtakatifu ndani ya kanisa ulifanya karismatiki ya kipentekoste kuenea na hivi hata baadaye baadhi ya wakatoliki kama wale walioshiriki wikiend ya Dequene kuombewa Roho Mtakatifu na madhehebu ya kipentekoste. Huu ni kwa hakika Uekumene wa kiroho kwani tunashirikishwa vipawa vya Mungu kwa namna ambavyo Mungu mwenyewe amekusudia.
Ni vyema Karismatiki Katoliki ikaendelea kujiimarisha zaidi katika kuhubiri injili, kujifunza mafundisho ya kanisa na kuhimiza yale yanayotoka kwa mababa wa kiroho bila kupuuza.

Comments
Post a Comment